Kategoria kuu za mashairi

Mashairi huweza kugawika katika
kategoria mbili kuu:

1) Mashairi ya jadi

2) Mashairi huru

Mashairi ya jadi.

Mashairi haya pia huitwa mashairi ya kimapokeo au ya kiarudhi. Aina hii ya

mashairi hufuata kaida za utunzi wa mashairi. Kanuni hizi ni kama vile:

• urari wa vina

• mpangilio maalum wa beti

• mishororo sawa katika kila ubeti

• mizani inayojitosheleza katika
kila mshororo

• vipande sawa katika kila mshororo n.k.

Malenga wanaoshikilia msimamo huu huitwa wanamapokeo. Mashairi yasiyofuata sheria hizi hujulikana
kama guni. Mfano wa shairi la kiarudhi ni
kama lifuatalo.

Naja sasa ni ndiyani, naja kwetu Mzalendo

Naja nirudi nyumbani, nilowekwa nako kando

Kwetu’ mi nakutamani, kulo na mwingi uhondo

Nijaye ni yule nyundo, misumari hadharini

Naja kwingine kuwapi, kulojaa langu pendo?

Huenda nende kwinginepi, sawa nako kwa muundo?

Kaa kwingine anapi, ela kwenye lakwe gando?

Nijaye ni ile nyundo, misumari hadharini

Naja nije rudi papo, panigedeme mgando

Ningaambwa kwetu hapo, kwamba kwanuka uvundo

Sitakwenda penginepo, tarudi kuko kwa mwando

Nijaye ni ile nyundo, misumari hadharini

(Limenukuliwa)

Tunaainisha shairi hili kama la jadi kwa sababu:

• Lina urari wa vina; ubeti wa 1 vina ni………‘ni’………….‘ndo’

ubeti wa 2
……………………‘pi’…………….‘ndo

ubeti wa 3
……………………‘po’……………‘ndo’

         Lina mishororo sawa (minne) katika kila ubeti

         Mizani inajitosheleza katika kila mshororo (mizani 16)

         Vipande ni sawa (viwili, yaani ukwapi na utao) katika kila mshororo

         Lina beti tatu zinazojitosheleza.

Mashairi huru

Ni kategoria ya mashairi yasiyozingatia kanuni za utunzi. Hii ina maana ya kwamba kanuni zilizoorodheshwa chini ya mashairi ya kimapokeo siyo lazima zifuatwe. Aghalabu mashairi haya huzingatia maudhui kwa kina. Kila malenga huwa na mtindo wake tofauti wa kuwasilisha kazi yake. Wanaoshikilia msimamo huu nao huitwa wanamapinduzi. Mashairihaya pia huitwa mapingiti/mavue/masivina/zuhali/za kimapinduzi. Hebu tazama shairi lifuatalo.

Nimeyaandika maneno haya kwa niaba ya,

Mamilioni wasio malazi

Wazungukao barabarani bila mavazi

Wabebao vifurushi vilivyo wazi,

… milki yao ya maisha.

Kwa niaba ya:

Maelfu wanaovuma bila haki

Wiki baada ya wiki

Leo sumu au spaki

Leo kamba au bunduki

Na kwa wale wanasubiri kunyongwa

Kwa niaba ya

Vijana walio mtaani

Wale mayatima na maskini

Wazungukao mapipani

Kila pembe mjini

Kuokota sumu kutia tumboni

Kujua bila kujua

’ili kupata kuishi.

Kwa niaba ya:

Wakongwe wasiojiweza

Walao chakula kilichooza

Wachukuao choo wakijipakaza

Pole pole wakijiangamiza

Katika vyumba vyao

Baridi na giza

Kwa saba hawan watazama

Wala wauguza

Mbona tukasema kuwa shairi hilo ni huru?
Ni kwa sababu;

         Halina urari wa vina

         Mizani si sawa katika mishororo yake

         Idadi ya mishororo katika beti ni tofauti

Sifa za mashairi huru

         Huwa hayazingatii idadi sawa ya mishororo katika beti.

         Aghalabu huwa hayana urari wa vina.

         Hayana idadi maalum ya vipande katika mishororo.

         Huwa hayana idadi sawa ya mizani katika mishororo.

         Nyingi yazo huwa na kipande kimoja tu.

         Hutumia mistari mishata.

         Hayana kibwagizo bali huwa na kituo.

         Hutumia takriri kwa wingi.

 

    USHAIRI

1.        Historia ya Ushairi

2.        Changamoto za ufundishaji na usomaji wa uhairi

3.        Istilahi zinazotumika katika ushairi

4.        Sifa za mashairi ya kimapokeo

5.        Sifa za mashairi huru

6.        Bahari za mashairi

7.        Uchambuzi wa mashairi

8.        Uhuru wakishairi

 

hati miliki zimehifadhiwa

Leave a Reply

scroll to top