MBINU ZA TAFSIRI

 Zipo njia mbalimbali ambazo hutumika katika kutafsiri, baadhi ya njia hizo ni kama vile:

(i) Tafsiri ya neno kwa neno. [Word to word translation]

(ii) Tafsiri sisisi.[ Literal translation]

(iii) Tafsiri ya kimaana/uwazi.[ Semantic translation]

(iv) Tafsiri ya kimawasiliano.[Communicative translation]

(i) Tafsiri ya neno kwa neno [Word to word translation]

Hii ni aina ya tafsiri ambayo mofimu na maneno hufasiriwa yakiwa pweke pweke kwa kuzingatia maana zake za msingi bila kujali muktadha. Katika aina hii ya tafsiri mpangilio wa mofimu na maneno wa lugha chanzi hubakia vilevile bila kubadilika. Na kwa kawaida matini inayotafsiriwa huandikwa chini ya matini ya lugha chanzi. Tazama mifano ifuatayo ya tafsiri ya neno kwa neno:

Kiswahili: Alisoma hadi asubuhi

Kingereza: He/past/study/until/morning

Kiswahili: Alikimbia mpaka ofisini kwake

Kingereza: He/past/run/until/office/his

Kiswahili: Anasoma kitabu changu

Kingereza: He/present/book/my

Kiswahili: Walikula chakula chote

Kingereza: They/past/eat/food/all

Umuhimu wa njia hii, humsaidia mtu kuelewa muundo wa lugha chanzi na jinsi lugha chanzi inavyofanya kazi, kaina hii ya tafsiri hutumiwa na wataalamu wa lugha kuonesha namna maumbo au muundo wa lugha chanzi ulivyo, lakini mapungufu yake ni kuwa, aina hii ya tafsiri huwa haitoi maana inayokusudiwa kwa uwazi zaidi.

(ii) Tafsiri sisisi [ Literal translation]

Hii ni aina ya tafsiri ambayo maneno hufasiriwa yakiwa pweke pweke kwa kuzingatia maana za msingi katika lugha chanzi bila kujali sana muktadha lakini ni tafsiri inayofuata mfumo wa kisarufi hasa kipengele cha kisintaksia ya lugha lengwa. Ebu tuangalie mifano ifuatayo:

Kingereza: He was taken at the Central Police Station

Kiswahili: Alipelekwa kwenye kituo cha kati cha police.

Badala ya kuwa: Alipelekwa kituo kikuu cha polisi

(iii) Tafsiri ya kisemantiki/maana au uwazi [Semantic Translation]

Hii ni aina ya tafsiri ambayo mfasiri huegemea zaidi kwenye lugha chanzi. Katika aina hii ya tafsiri, mfasiri hufasiri kila neno katika sentensi jinsi lilivyo lakini kwa kufuata sarufi hususani vipengele vya kisemantiki na kisintaksia ya lugha chanzi. Inaitwa tafsiri ya kisemantiki kwa sababu, mfasiri anapofasiri hutakiwa kuweka mkazo kwenye maana ya matini kama ilivyokusudiwa na mwandishi wa matini chanzi.

Katika aina hii ya tafsiri, masahihisho au urekebishaji wa neno au jambo lolote unalodhani limekosewa haliruhusiwi isipokuwa unaweza kuweka hayo marekebisho au ufafanuzi katika tanbihi. Sasa tuangalie baadhi ya mifano ya aina hii ya tafsiri:

Kiswahili: Alikwenda mpaka hospitali

Kingereza: He went up to hospital

Kingereza: Jane married John

Kiswahili: Jane alimwoa John

Aina hii ya tafsiri, ina faida kubwa katika ukuaji wa lugha lengwa kwa kuingiza miundo ya misemo kutoka lugha chanzi, mathalani, lugha ya Kiswahili imepokea miundo mipya ya misemo kutoka lugha ya Kingereza, baadhi ya miundo hiyo ni kama vile:

Kiswahili: Usiku mwema ? kutoka Kingereza: Good night

Kiswhili: Mabibi na mabwana ? kutoka Kingereza: ladies and gentlemen

Kiswahili: Wako mtiifu ? Kutoka Kiingereza: Yours Sincerel

Kiswahili: Naomba nichukue nafasi hii.. ? Kutoka Kiingereza: May I take this opportunity…

[Tazama pia Mwansoko na wenzake: 2006]

(iv) Tafsiri ya kimawasiliano/ huru [Communicative Translation]

Hii ni aina ya tafsiri inayomlenga msomaji [hadhira] wa matini lengwa, ambaye katika aina hii ya tafsiri hatarajii kukutana na ugumu wowote katika matini atakayoisoma, bali hutarajia kukutana na tafsiri nyepesi ya dhana za kigeni katika utamaduni na lugha yake kwa kadiri itakavyoonekana. Hivyo basi, mfasiri wa aina hii ya tafsiri yuko huru kutafuta maneno na mafungu ya maneno yanayolingana na maneno, methali, nahau, utamaduni na mazingira ya lugha lengwa, pamoja na kuwa tafsiri ya kimawasiliano kufuata sarufi ya lugha lengwa ni lazima pia ifuate utamaduni, mazingira na historia ya jamii ya lugha lengwa. Tuangalie mifano ifuatayo:

Kingereza: Jane married John

Kiswahili: John alimwoa Jane

Kingereza: No need to cry over spilt milk

Kiswahili: Maji yakimwagika hayazoleki

Kiingereza: What comes around goes arround

Kiswahili: Mla vya watu, naye vyake huliwa.

Kiswahili: Akufaaye kwa dhiki ndiye rafiki wa kweli

Kiingereza: A friend in need is a friend in need

Kiswahili: Bahati haiji mara mbili

Kiingereza: Golden chance never comes twice

Aina hii ya tafsiri hulenga kutoa athari ile ile au inayokaribiana kwa hadhira ya matini lengwa kama ilivyo kwa hadhira ya matini chanzi[ matini asilia], hii ni aina ya tafsiri ambayo hutumika sana kufasiri mawazo ya kigeni katika lugha na mazingira mapya, mawazo ambayo huelezwa katika misingi ya lugha, utamaduni na mazingira yanayoeleweka kwa hadhira ya matini lengwa.

Ebu tuangalie baadhi ya mifano tuliyoiangalia katika tafsiri ya Kisemantiki [maana] tunavyoweza kutafsiri katika njia ya tafsiri ya kimawasiliano:

Kiingereza Kiswahili

Good night Lala salama

Ladies and Gentlemen Ndugu zangu

Yours Sincerely Ni mimi

May I take this opportunity to… Naomba mnisikilize

Hivyo basi, katika aina hii ya tafsiri, mfasiri hutafuta methali au misemo inayopatikana katika lugha lengwa inayohusiana au kukaribiana na ile ya lugha chanzi. Ebu jaribu kutafsiri misemo/methali zifuatayo ya lugha ya Kiswahili kwenda lugha ya Kiingereza:

Adhabu ya kaburi aijuaye maiti

Asiyekubali kushindwa si mshindani

Asiyefunzwa na mamaye hufunzwa

Chema chajiuza kibaya chajitembeza

Dua la kuku halimpati mwewe

Bandubandu humaliza gogo

Jogoo wa shamba hawiki mjini

La kuvunda halina ubani

Mtegemea cha nduguye hufa masikini

Faida ya aina hii ya tafsiri, humfanya mfasiri kuwa huru kutumia maneno au mafungu ya maneno ambayo huweza kutoa athari ile ile au inayokaribiana na maneno au mafungu ya maneno katika matini ya lugha chanzi, lakini mapungufu ya aina hii ya tafsiri huweza kutokea iwapo mfasiri ataamua kuegemea mno kwenye mawazo, historia, mazingira au itikadi ya lugha lengwa. Ebu tuangalie mifano ifuatayo:

Kingereza: The Merchant of Venice

Kiswahili: Mabepari wa Venisi

Ukiangalia mfano huo utaona kuwa, The Merchant of Venice, tamthiliya iliyoandikwa na William Shakespeare, ingefaa pia kufasiriwa kuwa, Wafanyabiashara wa Venisi, lakini Mwalimu J.K Nyerere aliamua kuifasiri kuwa, Mabepari wa Venisi kutokana na kuwa Nyerere ndiye mwasisi wa itikadi ya Ujamaa nchini Tanzania, hivyo aliegemea katika itikadi kufasiri.

Hivyo basi, mtu anapokuwa anafanya kazi ya kufasiri, maandishi yo yote kutoka lugha moja kwenda lugha nyingine atajikuta akiangukia katika moja wapo ya njia tulizozijadili hapo juu, lakini ikumbukwe tafsiri ya neno kwa neno ni nadra sana kutumiwa na wafasiri wengi, na njia hizo huweza kuingiliana katika matini moja ya tafsiri.

Ukalimani [Interpritation]



MAREJEO

Cartford [1995] A linguistic Theory Translation

Mwansoko, H.J.M na wenzake [2006] Kitangulizi cha Tafsiri, Nadharia na

Mbinu.TUKI.Dar-es-salaam

Newmark, P [1982] Approaches to Translation, Oxford, Pergamon Press

Newmark, P [1988] A Text book of Translation, London, Prentice Hall.

Oxford University Press Dar-es-salaam

Semzaba, E [2006] Ngoswe, Penzi Kitovu cha Uzembe. The General Booksellers LTD.

D.S.M

TUKI [2002] Kamusi ya Kiswahili Sanifu. TUKI, Dar-es-salaam

TUKI [1985] Kiswahili, Jarida la Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili.

www.bakita.org.tz retrieved on Monday 04th July 2018

www.jim-mission.org.uk retrieved on Monday, 04th July 2018

www.ajol.inf retrieved on Monday, 04th July 2018

Vitabu vilivyotafsiriwa ambavyo vimetumika kama marejeo

Ayi Kwei Armah, Wema Hawajazaliwa, kimetafsiriwa na Abdilatif Abdalla

Ferdinand Oyono: House boy, Kimetafsiriwa na Raphael Khasao na Nathan Mwele.

William Shakespeare: Juliasi Kaizari: Kimetafsiria na Julius K. Nyerere

Mabepari wa Venisi: Kimetafsiriwa na Julius K. Nyerere

Hekaya za Abunuwasi: Kimetafsiriwa na Interterritorial Language Committee, East Africa

Alfu Lela Ulela: Kimetafsiriwa na Sir Richard Burton

Sir Rider Haggard: Mashimo ya Mfalme Suleiman


hati miliki zimehifadhiwa

Leave a Reply

scroll to top