Viambishi Awali

Viambishi awali Hivi hupachikwa kabla ya mzizi wa neno na huwa ni vya aina tisa:-

i.    Viambisha awali vya nafsi– hivi hudokeza upatanishi wa  nafsi katika kitenzi, zipo nafsi tatu, nafsi ya kwanza, ya pili, na ya tatu na viambishi vifuatavyo huwakilisha nafsi hizi:

NafsiUmojaUwingi
Ya kwanzaNi-Tu-
Ya piliU-M-
Ya tatuA-Wa-

Mfano katika neno :

NafsiUmojaUwingi
Ya kwanzaNi-nasomaTu-nasoma
Ya piliU-nasomaM-nasoma
Ya tatuA-nasomaWa-nasoma

ii.  Viambishi awali vya ngeli– hivi hupatikana mwanzoni mwa nomino au vivumishi ili kudokeza hali ya umoja na uwingi.

Mfano:-Mtu (umoja) – Watu (uwingi)

         Msafi (umoja) – Wasafi (uwingi)

iii.   Viambishi awali vya ukanushi – hivi hudokeza hali ya uhasi wa tendo. Huwakilishwa na mofimu (ha-) na (si-)

Mfano:- Amekula (uyakinifu) – Hajala (ukanushi), Nakula (uyakinifu) – Sili (ukanushi)

iv.   Viambishi awali vya Njeo- hivi hudokeza nyakati mbalimbali ambazo ni wakati uliopita, uliopo na ujao.

NyakatiMofimu
UliopoNa-
UjaoTa-
UliopitaLi-

Mfano:- Mlituona

               Utakuja

v.  Viambishi awali vya hali- hivi hudokeza hali mbili za nyakati ambazo ni mazoea ambayo huwakilishwa na mofimu {hu} na timilifu inayowakilishwa na mofimu {me}.

Mfano:-Hucheza

         Amelima

vi. Viambishi awali vya masharti – Hivi hudokeza hali ya masharti au uwezekano katika tendo. Mofimu hizo ni kama –ki-, nge-, ngali- n.k.

Mfano:- ukija

           Ungekuja

           Angalimkuta

vii.  Kiambishi cha urejeshi wa mtenda (kiima) – Hiki hudokeza urejeshi wa nomino inayotenda katika kitenzi.

Mfano: – Aliyekuja {-ye-} hudokeza urejeshi wa mtenda.

viii.  Kiambishi kiwakilishi cha mtendwa au mtendewa (shamirisho) – hivi huwakilisha mtendwa au mtendewa wa jambo.

Mfano; Nilimpiga, Uliukata, Nimeipenda, Wameniteta.

ix.   Kiambishi awali cha kujirejea (kujitendea) – hiki huwakilishwa na mofimu (-ji-)

Mfano; kujipenda